Mwl El Olam Lwoga.

Mwl El Olam Lwoga.

Share

Mafundisho ya neno la Mungu, na huduma ya kiroho. Mathayo 4:4.

"...mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu"

Mawasiliano 0768363808.

19/06/2026

Siku ya 3.
Somo:UTUKUFU WA MUNGU.
HAGAI 2:9.
"Utukufu wa mwisho wa nyumba hii utakuwa mkuu kuliko utukufu wake wa kwanza, asema BWANA wa majeshi...".

*Ikiwa haujajifunza somo hili kwa siku 2 zilizopita ni vyema ukarudi kusoma toka mwanzo ili tuendelee kujifunza pamoja kwa mtiririko wa somo hili tulilofunuliwa na Roho Mtakatifu.

Leo tutajifunza kwa kuanza kuyaangalia...
MAMBO YANAYOMFANYA MUNGU ATUKUZWE KUPITIA MIMI NA MIMI NIPATE KUNUFAIKA KWA MUNGU KUTUKUZWA KUPITIA MIMI.

1.Uhusiano wangu mimi na Mungu.
uhusiano ni ushirika baina ya watu wawili au zaidi unaowaweka kuwa pamoja, huku ukiwa umebebwa na makubaliano fulani waliyopatania kuyafanya wakiwa pamoja.

kwa lunga nyingine ni kwamba hakuna uhusiano au ushirika unaowaweka watu kuwa pamoja ikiwa hakuna makubaliano waliyopatania kuyafanya wakiwa pamoja.
hivyo makubaliano na mapatano ndiyo yanayoleta uhusiano au ushirika kati ya mtu Mungu, mtu na mtu, watu na watu, nchi na nchi, kanisa na kanisa n.k.

*Shika:kwakuwa makubaliano na mapatano ndiyo yanayounganisha uhusiano au ushirika kati ya mtu na Mungu, mtu na mtu, watu na watu, nchi na nchi.
hayo makubaliano na mapatano yanapovunjika (kutokufanyika k**a walivyokubaliana na kupatana), uwe na uhakika huo uhusiano au ushirika wao utavunjika.

kwanini uvunjike?
Kwasababu kilichowaunganisha wakawa na uhusiano au ushirika wa pamoja ni makubaliano waliyokubaliana na mapatano waliyopatania kuyafanya wakiwa pamoja.
Amosi 3:3.
"Je! Watu wawili waweza kutembea pamoja, wasipokuwa wamepatana?"

Kumbuka:kwakuwa Mungu ni Roho asiye na mwili, hivyo mtu anapokubaliana na kupatana kuwa na uhusiano na Mungu, Mungu huingia ndani yake na kutembea pamoja naye, akiambatana naye ili kumsaidia kuyatenda yale yote waliyokubaliana na kupatania.
Yohana 4:24, 1 Wakorintho 3:16.

Shika:"uwepo wa Mungu upo Kila mahali, lakini si kila kitu huubeba huo uwepo wa Mungu"
kwa maana nyingine ni kwamba Roho wa Mungu yupo Kila mahali, lakini Roho wa Mungu hakai ndani ya kila kitu"
Zaburi 139:7,8.

"Roho wa Mungu au uwepo wa Mungu hukaa ndani ya mtu mtakatifu pekee".
ni neema na raha iliyoje, katika vitu vyote alivyoviumba Mungu, Mungu anatafuta mtu atakayekuwa tayari kumkubalia ili akae ndani yake.
Isaya 66:1,2, 1 Wakorintho 3:16,17.

kumbuka:"Roho wa Mungu au uwepo wa Mungu unaweza kukaa juu ya kitu chochote, na hicho kitu kikatumika kwa kulitimiza kusudi la Mungu, na Mungu akatukuzwa kupitia hicho, lakini hicho kitu kisinufaike kwa chochote, kwa Mungu kutukuzwa kupitia chenyewe (hicho kitu kikatumika bure, pasipo kupata malipo yeyote kwa Mungu)".
hivyo ili mimi nipate kunufaika kwa Mungu kutukuzwa kupitia mimi, yanipasa kila nifanyapofanya jambo analolitaka Mungu nilifanye, nihakikishe ninalifanya huku uwepo wa Mungu ukiwa pamoja na mimi ndani yangu (Roho wa Mungu yupo ndani yangu), na siyo uwepo wa Mungu kunijia ukanikalia ili kumdhihirisha Mungu apate kutukuzwa katika jambo ninalolifanya na baadaye ukaondoka.

*uhusiano wa mtu na Mungu unapovunjika, Roho wa Mungu huondoka ndani ya huyo mtu.
Matendo 5:32.
-Mungu anachokitaka kwangu ni nimtii yeye kwa kuyafanya yale yote anayoyataka niyafanye k**a vile makubaliano na mapatano yetu yalivyokuwa mwanzo wa uhusiano wetu.

Roho wa Mungu anapokaa ndani ya mtu, huumbika ndani ya huyo mtu, kwa kuwekeza roho zake ndani yake (Isaya 11:2), ili apate kutenda kazi pamoja na huyo mtu katika yale anayoyataka ayafanye kwaajili ya utukufu wake (1 Wakorintho 3:9).
'huku ni kutengenezwa au kuandaliwa
kwa mtu kwaajili ya kufaa kuyafanya yale aliyomkusudia Mungu ayafanye'.

Mungu anapoumbika vya kutosha ndani ya mtu au anapojaa ndani ya mtu, haishii tu kujaa ndani yake, bali hutoka ndani yake na kufurika katika mwili na vilivyo katika mwili wake, ili apate kujitukuza kwa kutenda kazi kwa haraka na uwazi zaidi.
pia Mungu anapoumbika vya kutosha ndani ya mtu, ule ubinadamu wa mtu hufa, na Mungu kuishi ndani yake, na kutenda kazi ndani yake.
yaani Mungu mwenyewe ndiye anaishi na kutenda kazi ndani ya mtu.

*kumbuka: ili Mungu aumbike vya kutosha ndani ya mtu, na kujidhihirisha nje kwa uwazi zaidi, inategemea na kiwango cha uhusiano wa karibu kati ya mtu binafsi na Mungu (kiwango cha ushirika, kati ya mtu binafsi na Mungu).

Mfano:
1.Roho wa Mungu au uwepo wa Mungu katika vazi la Eliya.
2 Wafalme 2:9-14.
Elisha aliomba, mara dufu ya sehemu ya roho iliyokuwa ndani ya Eliya.
je! vazi la Eliya linahusiana vipi na roho iliyokuwa ndani ya Eliya? Kwasababu tunamuona Eliya anamjibu kuwa akimuona wakati akiondoka kwenda mbinguni, basi Elisha atapokea mara dufu sehemu ya roho yake .
Na ulipofika wakati wa Eliya kuondoka na kwenda mbinguni, Eliya alimuachia Elisha mavazi yake...na tunaona baadaye udhihirisho wa Mungu ukitembea na Elisha kwa mavazi ya Eliya.

2.Roho wa Mungu au uwepo wa Mungu katika vazi la Yesu.
Marko 5:25-34.
kutokana na Yohana 6:63 inasema 'Roho ndiyo itiayo uzima'.
je! Kuna uhusiano gani kati ya Roho kuachilia uzima kwa yule mwanamke aliyetokwa na damu muda wa miaka kumi na miwili na vazi alilolivaa Yesu?

3.Roho wa Mungu au uwepo wa Mungu katika mifupa ya Elisha.
1 Wafalme 13:20,21.
Kuna uhusiano gani kwa mtu aliyekufa kufufuka baada ya mwili wake kugusana na mifupa ya marehemu Elisha?

Mungu akubariki kwa kuendelea kujifunza.
Tukutane tena wakati mwingine.
Roho Mtakatifu ni mwaminifu tunaamini atazidi kutufundisha zaidi na zaidi.
Kwa maswali, maoni, ushauri karibu sana.

18/06/2026

Siku ya 2.
Somo:UTUKUFU WA MUNGU.
HAGAI 2:9.
"Utukufu wa mwisho wa nyumba hii utakuwa mkuu kuliko utukufu wake wa kwanza, asema BWANA wa majeshi...".

*Ikiwa haujajifunza somo hili kwa siku ya 1 ni vyema ukarudi kusoma toka mwanzo ili tuendelee tukijifunza pamoja kwa mtiririko wa somo hili tulilofunuliwa na Roho Mtakatifu.

Leo tutajifunza kwa utangulizi tu...
MAMBO YANAYOMFANYA MUNGU ATUKUZWE KUPITIA MIMI NA MIMI NIPATE KUNUFAIKA KWA MUNGU KUTUKUZWA KUPITIA MIMI.
(Yapo mambo ma 3 tuliyofunuliwa).

Kwanza kabisa ni muhimu sana kuelewa vizuri kichwa cha ujumbe kabla ya kuyaangalia hayo mambo ma 3...

"Anachokitaka Mungu kutoka kwangu ni Mungu afanye kazi pamoja na mimi ili ajitukuze duniani na mimi nifaidike kwa kuyapata yale aliyokwisha kuyaandaa kwaajili yangu".

1 Wakorintho 3:9.
-"tunafanya kazi tukiwa pamoja na Mungu (Mimi na Roho wa Mungu tumeunganika kuwa roho moja 1 Wakorintho 6:16,17).
-sisi ni shamba la Mungu (Roho wa Mungu anapokaa ndani yangu anawekeza vitu vyake ndani yangu, ili kupitia hivyo apate kujitukuza).
-Jengo la Mungu (Nyumba, Roho wa Mungu anakaa ndani yangu)".

Warumi 8:28.
-"Mungu anatenda kazi na sisi tunaompenda na kuna mambo mema aliyoyaandaa kwaajili yetu kwa sisi kukubali kutenda kazi na yeye ili ajitukuze kupitia sisi".

Waefeso 1:17,18.
-"tunapopata ufunuo na kumjua Mungu...
macho yetu ya rohoni yanatiwa nuru, tunaanza kuyaona mambo katika mtazamo wa Mungu mwenyewe au k**a anavyoona Mungu mwenyewe.
na tunapoona tunaanza kujua sababu ya Mungu kutuita (tumtumikie na tunufaike kwa kwenda mbinguni)...na pia tupate kujua yale Mungu aliyotuandalia ili tuyapate kutokana na wito tulioitiwa wa kumtumikia yeye.
hivyo tunapoyajua hayo ndipo tunapata nguvu ya kutokuchoka kuendelea kumtumikia Mungu, kwasababu tunalo tumaini la kupata kunufaika kwa Mungu kutukuzwa kupitia sisi.

*"utumishi wetu kwa Mungu siyo wa bure".
kwa lugha nyingine, unapomtumikia Mungu Mungu anakulipa kutokana na kazi ya utumishi wako uliyoifanya kwake".
hujawahi kusikie msemo wa 'hakunaga kazi ya bure' huu msemo ni halisia.

Tafakari:Ikiwa shetani anawalipa mema wale wanaomtumikia kwa uaminifu, je! si zaidi Mungu aliye mmiliki wa vitu vyote kutulipa na sisi tunayemtumikia yeye kwa uaminifu?

Ufunuo 22:12, 1 Wacorintho 3:13-15 (ahadi ya kulipwa kwa kwenda mbinguni na kupata taji).
Mathayo 19:27-29 (ahadi ya kukipwa duniani na mbinguni).

*Yesu hakufanyika maskini ili tukawe matajiri mbinguni, kwa lugha nyingine ni kwamba mbinguni hatutakwenda kurithishwa utajiri...2 Wakorintho 8:9, Waefeso 1:18.

Shika:ukifanya kazi pamoja na Mungu kwa uaminifu hakika Mungu atakulipa mema...ila usiifanye kazi ya Mungu ukitegemea kulipwa na mtu...mwenye kutulipa ni Mungu mwenyewe anayetupatia kazi.
Kwa lugha nyepesi ni kwamba muajiri wetu ni Mungu na kila mtu anategemea kulipwa na Mungu kutokana na kazi aliyoifanya (boss wetu ni Mungu pekee).

Kumbuka:siku zote kinachomfanya mtu afanye kazi kwa juhudi pasipo kuchoka wala kukata tamaa ni malipo anayotarajia kulipwa na aliyempatia kazi (ni malipo ya kazi anayoifanya).

Mfano:Yesu Kristo.
Waebrania 12:2.
"...ambaye kwaajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidhatau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa Mungu.
-Furaha hiyo tunaipata Ufunuo 5:12.
"Uweza, utajiri, hekima, nguvu, heshima, utukufu na baraka.

Mungu akubariki sana kwa kuendelea kujifunza.
huo ni utangulizi tu tuliojifunza...tukutane kwa wakati mwingine tena, tunamuamini Roho Mtakatifu atatufundisha zaidi hatua kwa hatua hata tutafikie kuyajua yale yote yaliyo ndani ya moyo wa Mungu katika somo hili.
Kwa maswali, maoni, ushauri karibu sana.

Photos from Mwl El Olam Lwoga.'s post 17/06/2026

Siku ya 1.
Somo:UTUKUFU WA MUNGU.
HAGAI 2:9.
"Utukufu wa mwisho wa nyumba hii utakuwa mkuu kuliko utukufu wake wa kwanza, asema BWANA wa majeshi...".

Maana halisi ya 'utukufu wa Mungu'
ni uwepo wa Mungu unaodhihirisha ukuu, heshima, nguvu na uweza wa Mungu (unaomdhihirisha Mungu).

1 Samweli 4:19-22.
4:21"Akamwita mtoto, Ikabodi, akisema, Huo utukufu umeondoka katika Israeli; kwa sababu sanduku la Mungu lilikuwa limetwaliwa...".
-Hilo sanduku la Mungu (sanduku la agano) kwa taifa la Israeli lilikuwa likiwakilisha uwepo wa Mungu kuwa katikati yao, na utukufu wa Mungu ulikuwa ukidhihirika kupitia hilo sanduku la Mungu.

Hivyo mahali uwepo wa Mungu upo, inamaanisha kuwa Mungu au Roho wa Mungu yupo hapo.

Shika hili:Nia iliyomsukuma Mungu kuumba dunia na vitu vyote vilivyomo ndani ya dunia (nikiwepo na mimi mwanadamu) ilikuwa ni ili Mungu ajipatie utukufu kupitia hivyo alivyoviumba.
Isaya 6:1-3, Mwanzo 1:31.
dhambi ilipoingua duniani na mwanadamu kuyatenda yaliyo maovu, yanayouondoa utukufu wa Mungu aliotaka Mungu aupate kutoka kwa huyo mwanadamu, kwa rehema za Mungu bado Mungu alimtafuta mwanadamu na kumuokoa kutoka katika dhambi na kumfanya kuwa wake ili aendelee kujipatia utukufu kutoka kwake.

Hivyo nia ya Mungu kuniokoa mimi ilikuwa ni ile ile yaani Mungu ajipatie utukufu kupitia mimi.
1 Wakorintho 6:19,20.
Good news bible inasema "mmenunuliwa kwa bei kubwa.kwa hiyo itumieni miili yenu kwaajili ya kumtukuza Mungu".
Isaya 43:7 inaeleza pia.

Tafakari:Ni mambo gani ninayoyafanya yanayomtukuza Mungu, au ni mambo gani ninayoyafanya ambayo hayamtukuzi Mungu...yanipasa nikumbuke kuwa anachokitaka Mungu kutoka kwangu ni ajipatie utukufu kupitia mimi pekee...

***Kwa neema ya Mungu siku inayofuata Roho Mtakatifu atatufundisha zaidi, tutajifunza "MAMBO YANAYOMFANYA MUNGU ATUKUZWE KUPITIA MIMI NA MIMI NIPATE KUNUFAIKA KWA MUNGU KUTUKUZWA KUPITIA MIMI".

Kusudi kuu la Roho Mtakatifu kutufunulia somo hili ni ili tupate kujua ya kuwa katika siku hizi za mwisho Mungu anataka AUDHIHIRISHE UTUKUFU WAKE MKUU DUNIANI KUPITIA KANISA LAKE (MTU WAKE AU WATU WAKE) na si hivyo tu bali KANISA LAKE PIA LIPATE KUNUFAIKA KUPITIA UTUMISHI WAO UNAOMPATIA MUNGU UTUKUFU.

Mungu akubariki sana tukutane wakati mwingine tena...kwa maswali, maoni, ushauri ninakukaribisha pia.

17/06/2026
27/05/2026

Mungu anaweza yainua mawe yakaifanya kazi yake... Wainjilist msilale, ihubirini injili ya Kristo Yesu.

26/05/2026

YOHANA 17:4,5.
Yesu alipokuwapo hapa duniani akiishi, aliishi kwa kuyafanya mapenzi ya Mungu pekee (yampendezayo Mungu), na hakufanya kwa nafsi yake (kwa nia ya kutaka kujitukuza mwenyewe).
Yohana 8:28,29.
Bali yote aliyoyafanya Yesu, aliyafanya yale aliyoambiwa na Mungu ayafanye, ili Mungu mwenyewe ajitukuze kupitia yeye.

Na wakati wote, ili Mungu anitukuze mimi mtumishi wake, anachokitaka kwangu ni kwanza yeye Mungu atukuzwe kupitia mimi mtumishi wake...na ili Mungu atukuzwe kupitia mimi ni lazima:
"Niyafanye yanayompendeza Mungu/mapenzi ya Mungu (anayotaka Mungu niyafanye) na ninapoyafanya, niyafanye kwa nafsi yake Mungu, yaani kwa nia ya Mungu, ya yeye Mungu kutaka kujitukuza".

Hivyo ili Mungu anitukuze mim, anachokitaka kutoka kwangu ni mimi nimtukuze yeye.

"Tuishi kwa kumtumuza Mungu pekee, ili naye Mungu atutukuze...yaani Mungu akitukuzwa kwa kupitia mimi, kuna sehemu ya utukufu wake ananipatia na mimi".

02/05/2026

UJUMBE KWA KANISA LA TANZANIA.

TUJUE NA TUSIJISAHAU KUWA TUPO KATIKA SIKU ZA MWISHO, NA MUNGU AMETUKUSUDIA KANISA LA TANZANIA KULETA UAMSHO WA INJILI DUNIANI KOTE, KATIKA SIKU HIZI ZA MWISHO.

"Mungu ameliweka kanisa la Tanzania kwenye vipimo, ili ajipatie ambao hawatakubali kumsujudia shetani/miungu...ili kwa kupitia wao apate kujitukuza kwa mataifa yote kwa utukufu wake mkuu, katika hizi siku za mwisho...Mungu anataka ajitukuze ya kuwa yeye ni Mungu wala hapana mwingine zaidi yake".

Kutaendelea kutokea vita na ugumu katika maeneo yote (kihuduma, kiuchumi, kielimu, afya, ndoa, mahusiano, ndugu na ndugu, hata katika ufalme wa eneo husika) ili kulipinga kanisa lijisalimishe (to surrender) kwa shetani na kumuabudu yeye na siyo kumuabudu Mungu wa kweli.

shetani ameinuka kwa nguvu kubwa ili kuyumbisha sana imani ya kanisa kwa kupitia vita (vita vya imani) ili lisimuabudu Mungu wa kweli, kwasababu katika kumuabudu Mungu, kunajengeka ushirika wa mtu na Mungu...na kwa ushirika huo wa mtu na Mungu, ndipo Mungu anapomtengeneza mtu kwaajili ya kumtumia kwa utukufu wake.

LUKA18:7,8.
-Mungu hataacha kujifunua kwa wateule wake, yaani kanisa...lakini atakapokuja kuwachukua hao wateule (kanisa) je ataiona imani yao kwake? (ataona tegemeo lipo kwa Mungu?).
je ninamuabudu Mungu ili nipate vitu kwake? na huku imani yangu (tegemeo langu) halipo kwake?

Ninajiuliza, je naweza nikawa ninamuabudu Mungu lakini imani yangu ikawa haipo kwake?
jibu ni ndiyo...yaani naweza nikamuabudu Mungu kwasababu ninamjua kuwa yeye ndiye Mungu (yupo juu ya vyote) na ninamjua ya kuwa yeye ni Mungu, lakini hiyo imani yangu isiwe kwake (yaani ninamuabudu ili nijinufaishe na alivyo navyo).

YAKOBO 2:19.
-Imani bila matendo imekufa.
Imani huanzia rohoni, moyoni mwa mtu na kudhihirika mwilini katika matendo.
hivyo ukamilifu wa imani upo kwa kuanzia moyoni mwa mtu na kudhihirishwa katika matendo.
-imani isiwe tu moyoni na isidhihirishwe katika matendo...wala isiwe katika matendo huku moyoni imeondoka.
tusiwe k**a shetani anayeamini kuwa Mungu yupo na anatetemeka mbele za Mungu, lakini hayupo tayari kumuabudu Mungu na kumtii Mungu katika kutenda mema anayoyataka Mungu.

-Mungu anataka tuilinde imani yetu kwake.
Tusimuabudu tu Mungu kwa maneno na huku mioyoni mwetu hatujaiweka imani yetu kwake (hatujamfanya kuwa tegemeo letu/Mungu hayupo ndani yetu, tumefarakana naye kwa maovu yetu)...na tusimuabudu Mungu kwa maneno tu na huku ukiri wetu kwa matendo haupo kwake.
MATHAYO 15:8.
-Nisimuabudu Mungu kwasababu tu ananijibu maombi nimuombayo, bali nijitazame je imani yangu ipo kwa Mungu kweli?...kwasababu imani yangu ikiwa kwa Mungu, hakuna chochote kitakachonitenga na upendo wake (Warumi 8:35-39).
HIZI NI SIKU ZA MWISHO na Mungu analitengeneza kanisa kwa kulipima katika imani...ili ajipatie wamfaao yeye, watakaomdhihirisha kwa mataifa yote, mataifa wapate kumjua yeye na kumgeukia yeye (kutubu), na kukiri kuwa yeye ndiye Mungu wa kweli wala hapana Mungu mwingine astahiliye kuabudiwa...

Hivyo kumbuka hili kuwa "imani ya kanisa ipo kwenye kipimo" yaani kanisa ambalo ni mtu binafsi na siyo jengo au dhehebu fulani.
1 Timotheo 4:1.
-kusikiliza roho, na mafundisho ya mashetani siyo mpaka uhubiriwe na watu waliobeba roho na mafundisho ya shetani, bali shetani mwenyewe anaweza kukusikizisha sauti yake na mafundisho yake kupitia mawazo yako, kwa kusudi aiondoe imani yako kwa Mungu.

USIOGOPE, MUNGU YUPO TAYARI KUMLINDA YEYE AMBAYE MOYO WAKE UMEMTEGEMEA, yaani ambaye imani yake aneiweka kwa Mungu...katika vita na hatari zote zitakazojitokeza mbele yake...Mungu atamshindia.
ISAYA 26:3,4.

"inuka na umuite Mungu akusaidie utoke hapo ulipokwama na usonga mbele usikubali kufa huku imani yako kwa Mungu umeipotea"
AMINA.

15/04/2026

WAEBRANIA 10:38.
"LAKINI MWENYE HAKI WANGU ATAISHI KWA IMANI..."

08/03/2026

Naomba unisaidie tumcheke shetani na vibaraka wake 😂😂😂, maana ana hasara kwetu tuliokombolewa na YESU KRISTO.

Want your school to be the top-listed School/college in Dar es Salaam?

Click here to claim your Sponsored Listing.

Location

Category

Website

Address

Mbezi
Dar Es Salaam